Head image
Govt. Logo

Hits 121563 |  21 online

           


DKT SHAJAK ATEMBELEA MRADI WA EBARR DODOMA.
news phpto

Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Dkt.Omari D Shajak akikagua mashine ya kukamua mafuta ya alizeti katika ziara ya kukagua Mradi wa Kuhimili Mabadiliko ya Tabianchi kwa kutumia Mifumo Ikolojia katika wilaya ya Mpwapwa mkoani Dodoma.

Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Dkt. Omar D. Shajak amefanya ziara ya kukagua Mradi wa Kuhimili Mabadiliko ya Tabianchi kwa Kutumia Mifumo Ikolojia Vijijini (EBARR) katika Wilaya ya Mpwapwa mkoani Dodoma.

Katika ziara hio amekagua miradi ya kisima, kitalu, nyumba katika Kijiji cha Ng’hambi, mashine ya kukamua mafuta ya alizeti, ujenzi wa kituo cha huduma za mifugo na lambo katika Kijiji cha Ng’hambi, ujenzi wa kisima pamoja na josho la kuogeshea mifugo katika Kijiji cha Kazania yenye thamani ya shilingi bilioni 1.2.

Akizungumza kwa nyakati tofauti wakati wa ziara hiyo, Dkt. Shajak ameishukuru na kuipongeza Ofisi ya Makamu wa Rais kwa kuratibu vyema mradi huo unaotekelezwa na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.

Lengo la ziara hio ni kuangalia hatua zilizofikwa katika utekelezaji wa Mradi wa EBARR kwa upande wa Tanzania Bara lakini pia kujifunza yale ambayo yamefanywa vizuri zaidi na Zanzibar wakaongeze juhudi na yale ambayo yanatekelezwa vizuri kuendelea na hakuna kurudi nyuma.

Dkt Shajak amewakumbusha wananchi kuwa msingi wa mradi sio kupata uhifadhi wa mazingira pekee bali Serikali inahakikisha kuwa wananchi wanapata kufanya shughuli zao za msingi za maisha hasa maji na kupata huduma ya maji kwa ajili ya kilimo, ufugaji na maji kwa ajili ya kuishi kwani maji ni uhai.

“Kila mradi unaokuja nyinyi wananchi ndio wahusika wakuu na serikali kazi yake ni kuratibu hivyo mnao wajibu wa kuilinda na kutunza rasilimali zilizopo pamoja na miundombinu iliyopo lazima tuitunze maana pia waliotusaidia hawawezi kutusaidia milele tukishakusaidiwa basi tuidumishe na kuzalisha miradi mengine” alisisitiza Dkt Shajak

Pia, Dkt. Shajak amewapongeza wasimamizi wa mradi huo wilayani Mpwapwa kwa kuisimamia vizuri na kuleta ufanisi kuanzia hatua ya ujenzi wake hadi kukamilika na kusema kuwa lengo la Serikali inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt Samia Suluhu Hassan ni kuhakikisha inawasaidia wananchi wake waweze kuwa na maisha mazuri licha kuwepo kwa changamoto za kimazingira.

Nao wanakijiji wa vijiji vilivyotembelewa na Katibu Mkuu wameishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuwapelekea mradi huo ambapo wameahidi kuuendeleza na kuutunza ili uendelee kuleta manufaa na tija zaidi.

Katika ziara hio Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Dkt Omar D. Shajak amefuatana na Mkurugenzi Idara ya Mazingira Bi Farhat Mbarouk, mratibu wa mradi EBARR Zanzibar Bw Alawi Haji Hija pamoja na viongozi mbali mbali kutoka Ofisi ya Makamo wa Rais Muungano na Mazingira.

Mradi wa kuhimili mabadiliko ya tabianchi na kurudisha uoto wa asili unafadhiliwa na Mfuko wa mazingira wa dunia (GEF) unatekelezwa katika wilaya za Mpwapwa (Dodoma), Simanjiro (Manyara), Mvomero (Morogoro) na Kishapu (Shinyanga) kwa upande wa Bara

Aidha kwa upande wa Zanzibar mradi unatekelezwa kwenye Mkoa wa Kaskazini Unguja ndani ya Wilaya ya Kaskazini “A” Kijiji cha Matemwe katika Shehia za Matemwe Kijini, Mbuyutende, na Jukakuu Wadi wa Kijini na unasimamiwa na Ofisi ya Makamo wa Rais Muungano na Mazingira kwa kushirikiana na Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais – Zanzibar.

Huduma za Tehama

Barua Pepe

Sisi

Mwanzo Kuhusu Sisi Idara Zetu

Viunga Muhimu

ZEMA ZAC DDA IKULU

Mawasiliano

Ofisi Kuu
S.L.P 2808, Migombani, Zanzibar
Tel.: +255(24)2232474 Mhe Waziri



Tel.: +255 (24)2232475 Katibu Mkuu,
Fax: +255 (24)2232476
Email: info@omkr.go.tz